0
Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini Kati, Dk. Solomon Masangwa amewataka waumini wa kanisa hilo kusimama katika imani zao wasidanganywe na manabii wa uongo wanaotoza waumini fedha.

Aidha amewataka waumini wa kikristo nchini kuishi kwa kuzingatia imani ya dini hiyo ili kuishi maisha yanayompendeza Mungu.

Dk. Masangwa ameyasema hayo leo Jumapili Aprili Mosi, mjini hapa alipokuwa akihubiri katika Ibada ya Pasaka iliyofanyika katika Usharika wa Mjini Kati Arusha na kuongeza kuwa kuna baadhi ya waumini ambao amewataka kuacha tabia ya kutanga tanga katika dini ambapo wamekuwa wakidanganywa na watu wanaojiita manabii na mitume.

“Kwanini mnakubali kudanganywa, siku hizi kuna watu wanajiita manabii, mitume na mnaenda kwao tena kwingine mnalipa kiingilio hata laki moja ili kumuona nabii au mtume,kwanini mdanganywe na mnasahau kusimama katika imani zenu,mnasahau ukombozi umepatikana kwa kifo na kufufuka kwa Yesu,” amesema.

Pamoja na mambo mengine, Askofu Masangwa amekemea vitendo vya uovu vinavyoendelea nchini ikiwamo mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi na wizi.

“Baadhi ya waumini wamekuwa wakitaka kuishi maisha mazuri, biashara zao kukua kwa kasi ambapo wengine wanajihusisha na imani za kishirikina zinazowafanya kujiingiza katika vitendo viovu.

“Kwanini mnakwenda kukata viungo vya albino au kumrusha mwenzao au kuiba, unakwenda kutafuta hirizi ili biashara ishamiriili maisha yawe mazuri mnasahau Yesu ni  bwana wa mabwana, Mungu ndiye anayetoa uwezo na nguvu za kuwa tajiri, mtegemeeni si waganga,” amesema.

Post a Comment

 
Top