0
Mbunge wa Tarime Vijijini kupitia tiketi ya CHADEMA, John Heche ameweka wazi kuwa kwa sasa ameanza kupata vitisho mbalimbali kutoka kwa watu wasiojulikana wakimtishia kumpoteza baada ya kusema ukweli kuhusu kupanda kwa gharama za vitambulisho vya Taifa.


Kupitia taarifa yake aliyoitoa kwa Waandishi wa Habari, John Heche amedai kuwa ameanza kupata vitisho hivyo ambapo amekiri haviwezi kumrudisha nyuma katika harakati kuisimamia na kuibana Serikali .

Mhe. Heche amesema vitisho hivyo vimekuja baada ya kutoa taarifa Bungeni kuwa serikali ilidanganya umma juu ya mradi wa e-passports na kupanda kwa gharama za vitambulisho vya Taifa.

Soma taarifa yake kamili hapa chini aliyoitoa kwa Vyombo vya Habari;

Vitisho dhidi yangu kuhusu mradi wa e-passports na vitambulisho vya Taifa:
Mtakumbuka kuwa juzi jioni nilizungumza bungeni kuhusu Serikali kudanganya umma Kuhusu mradi wa e-passports na kuhusu kupanda kwa gharama za vitambulisho vya Taifa. Maelezo yangu bungeni yalitokana na Taarifa kutoka Kamati ya PAC na yalijibiwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi.

Sasa ndugu zangu nimeanza kupata vitisho dhidi ya ‘credibility’ yangu na maisha yangu. Ndugu zangu Taifa letu linapitia wakati ngumu Sana.
Genge la wahalifu wa ki Uchumi na kisiasa kamwe lisitarajie nitatishika ama kubadili msimamo. Vitisho vilivyoanza dhidi yangu baada ya kuibua Ufisadi Katika Vitambulisho vya Taifa na E -Pasport havitaniogopesha kamwe. Njia zao ovu AMA kunitisha ama kutaka kuchafua Heshima yangu AMA kunitengenezea kesi AMA kuninifanyia alichofanyiwa mh Tundu Lisu hazitanirudisha nyuma. Leo nimepigiwa simu kipeperushi kinachojiita gazeti la Tanzanite kwa kutumia namba ya simu 0713295860 kusema eti nimehongwa ili kuzungumza nilichozungumza Bungeni. Hizi ni njama za kizamani kufunga watu midomo.

Ninahitaji mambo 2 tu, moja Serikali ionyeshe kuwa ilitoa kazi ya e-passports kwa zabuni na washindani walikuwa kina nani. Pia alichosema Rais ni kwa components zote 6 za mradi au ni kwa passport tu? Mbili, Serikali iweke wazi nyongeza ya mkataba ya vitambulisho vya Taifa na ieleze sababu za gharama ya kutengeneza kitambulisho kupanda kutoka shilingi 17,000 kwa kitambulisho Mpaka shilingi 26,000 kwa kitambulisho.

Serikali iache kunitisha. Naandaa nyaraka zote muhimu na nitapeleka Bungeni kuomba Kuundwa Kamati Teule ya kibunge juu ya ubadhirifu huu. Serikali itambue kuwa rasimu ya Taarifa ya PAC iliyonyofoa Taarifa kuhusu NIDA tunayo na tunajua njama zilizotumika kuondoa eneo hilo. Hata nikiuwawa Watanzania watajua ukweli tu kwani Taarifa hiyo ipo kwa wabunge wengi.
John Heche, Mb
Tarime Vijijini
3/2/2018

Post a Comment

 
Top